Friday, June 15, 2012

BARUA YA HERMY B KWA MILARD AYO




Kufuatia mahojiano kati ya kipindi cha Amplifaya cha Clouds Fm na Hamis Mwinjuma aka MwanaFA, Mwenyekiti mtendaji wa B’Hits Music Group Ltd, amemuandika barua mtangazaji wa kipindi hicho Milard Ayo kutoa ufafanuzi juu ya kilichoongewa na MwanaFA. Habari hiyo pia iliandikwa kwenye blog ya Milard tarehe 10, June, 2012. Wakati wa kutuma barua hiyo, Hermy B ametutumia pia na hivi ndivyo anavyosema:



Ningependa kutoa ufafanuzi wa habari iliyoandikwa na blog yako kufuatia mahojiano yako na mwana F.A. Nirejee kwamba mahojiano hayo yanasema kwamba Studio ya kurekodi muziki ya Kampuni ya Bhits imepandisha bei ya kurekodi, na bei hiyo ndiyo chanzo cha AY na F.A kuhamishia kazi zao sehemu nyingine.

Baada ya kusoma makala hiyo inayonihusu mimi binafsi na kampuni ya Bhits kwenye blog yako nimeona umuhimu wa kujibu makala yako kwani kwa mtu mwingine anaweza kuona ni kitu cha kawaida lakini kwangu naumia kwa sababu maneno hayo yameshaweka na yanaendelea kutia hofu wateja wangu hasa hawa wa muziki kwa kuwafanya wajihisi hawana hicho kiwango cha fedha, kurekodi muziki pale Bhits.

Naelewa kwamba maneno haya ya uongo mtupu yanatokana na mimi kama producer Bhits kushindwana biashara na AY na FA, lakini sioni sababu ya kuendelea kuongea maneno ya uwongo na kuniharibia biashara yangu. Sijui nimeawaudhi nini ndugu zangu hawa mpaka wanataka nionekane mimi nina tabia ya ulafi kwa wasanii wote hapa Tanzania.

Kitu ambachao hakifahamiki ni kwamba hata Mwana FA kama ilivyo kwa A.y nae alinitafuta kwa njia ya simu mwanzoni mwa mwaka huu akinitaka nimuuzie nyimbo zake alizorekodi kwangu kwa utaratibu wa reja reja kama vile alivyohitaji A.Y, lengo likiwa ni kuzindua albamu hiyo na kuiuza. Bei aliyotaka kulipa ilikua pia ni ile ile ya kujilinganisha na msanii mdogo anaehangaika kutoka.

Kitu kingine kilichofanya tushindwane kibiashara ni pale F.A alipodai bei hiyo ndogo itahusika katika kumuuzia pia haki zote za muziki huo, yani za kwake na zangu. Kwa namna nyingine niliombwa nikane haki zangu za muziki kama Producer na muziki huo uwe mali ya Mwana FA moja kwa moja, akiwa na haki ya kuuza, kuukodisha na kufanyia biashara yoyote ile anavojiskia yeye bila mimi kuhusika.

Na mimi nikitaka kutumia hata mdundo wa wimbo huo nitahitaji kumuomba ruhusa yeye labda hata kwa malipo na kinyume cha hapo ana haki ya kunipeleka mahakamani kunishtaki kwa wizi.

Nilishangazwa kwa kitendo cha FA kudhani kuwa naweza kukana haki zangu za kimuziki kwa sababu ya tamaa ya pesa ndogo, nasema kwamba ni hela ndogo ukilinganisha na thamani ya haki zangu za muziki ambazo huko mbele siwezi jua zitanisaidia vipi. Mabishano haya ya bei yaliendelea mpaka tukafika sehemu nikamwambia Mwana F.A anipe Milioni Moja kwa wimbo mmoja ataochukua kwangu kwa ajili ya albamu yake. Akanambia tuma mkataba lakini aliongeza maneno “bei yako sio ya kihalisia”. Mkataba huo ulikuwa na kifungu cha kudumisha urafiki wetu ambacho kinaeleza kuwa, “mauzo ya albamu ni mali ya msanii, akiamua kunipatia chochote hewala lakini mkataba huu haumlazimu”, lakini hakusaini mkataba huo.

Nachojiuliza neno kupandishiwa bei lina maana gani? Kwani si lazima uwe na bei ya mwanzoni ili inayofata iwe kubwa zaidi? Sasa kama wasanii hawa kwangu walikua wanarekodi bure na hawalipi hata senti ya umeme wala software ambazo mimi nimekua nazilipia hela nyingi kwa mwezi kuzifanya zipate leseni ya kufanya kazi watakua vipi na haki ya kusema wamepandishiwa bei?

Katika barua iliyopita nimesema kwamba fedha niliyopata kutokana na muziki wao haizidi milioni tatu kwa miaka yote minne niliyokuwepo nao.
Siifahamu na sijawahi kuwatajia hiyo bei ambayo inaweza kuwafanya A.Y na F.A warekodi nyimbo za kutosha hata nje ya Tanzania.

Bei ya Bhits wateja wake wanaifahamu na ipo pale pale kwa kila mtanzania kumudu. Ubora wa muziki wetu wasanii wanaujua pia na kwa anayependa kurekodi kwetu anakaribishwa kwa kuwa hatubagui na ambaye hajaridhika na viwango vyetu vya ubora na bei, hili ni soko huria anaweza kuchagua sehemu nyingine kwa amani kabisa.


Watu wanaweza wakaona mimi ni mchochezi na mgomvi lakini itambulike hili swala lilikwisha tokea February mwaka huu nikiwa mimi ndiye niliyeumizwa na nikaamua kukaa kimya. Nashindwa kuelewa kwa nini wao wameamua kuongelea makubaliano yetu binfasi kwa media tena kwa kuyageuza maneno.
Itambulike kuwa mara ya kwanza kabisa hili linasikika kwa media niliwatafuta kwa simu ndugu zangu hawa nikawaambia kuwa hakuna haja ya Kuongea kwa kuwa yameshakwisha tukae kimya tulindane. 
Lakini naona wanaendelea kuongea uongo huo ambao unaniumiza mimi na kampuni ya B Hits kibiashara.

Biashara zipo nyingi bado na labda huko mbele tutakutana tena, hakuna haja ya kuharibu kila kitu leo  kwa vitu vidogo kama hivi halafu kesho pia tupoteze nafasi ya kufanya mambo makubwa, ombi langu ni kwamba tuachane kwa amani. Haswa ukitegemea hatuna mkataba wa maandishi kati ya mimi, Mwana F.A na A.y nafikiri kuachana ni kitu rahisi na cha amani na kisichohitaji nguvu wala maumivu kukitimiza.

Namalizia kwa kusisitiza kuwa niliyoyasema ni ya ukweli na itakaponilazimu kutoa ushahidi nitafanya hivyo.

Wasalaam
Hermes Bariki Joachim (Hermy B)
Managing Director