Tuesday, July 10, 2012

WABUNGE JADILINI HOJA; MNACHUKIZA WANANCHI KWA VIJEMBE MNAVYOTOA



Spika wa Bunge, Anne Makinda.
TUKIWA katika hali ya kutafakari amani ya nchi hii, tumshukuru Mungu kwani bado anatupenda na tuzidi kumuomba ili atuepushie na mifarakano yoyote ambayo inaweza kugawa taifa letu.
Baada ya kusema hayo nizungumzie bunge letu tukufu linaloendelea kuketi mjini Dodoma katika kikao cha bajeti ya serikali.
Wiki iliyopita ndani ya bunge hilo tukio la kutekwa nyara na kuteswa kisha kuumizwa kwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk Steven Ulimboka, liliibua mgawanyiko mkubwa ndani ya kikao cha Bunge.
Tulishuhudia ‘laivu’ malumbano ya wabunge kutoka chama tawala CCM na Chadema, ambapo wawakilishi hao wa wananchi walishindwa kuficha hisia zao na tofauti kwa kila mmoja kuvutia upande wake.
Aliyeanzisha vuta nikuvute hiyo ni Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ kudai kuwa waliofanya kitendo hicho ni sawa na wanamgambo hatari wa Janjaweed wa Sudan.
Kauli yake ilizua tafrani kubwa ndani ya Bunge huku Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwezeshaji), Dk. Mary Nagu akiomba Mwongozo wa Mwenyekiti wa Bunge, Sylivester Mabumba aliyekuwa akiendesha kikao hicho.
Akichangia hotuba ya Ofisi ya Rais, (Utumishi, Utawala Bora, Ikulu na Mipango) Mbilinyi, alisema kitendo alichofanyiwa Dk.Ulimboka ni cha kinyama na baadhi ya watu wanaamini kwamba Serikali ilihusika. Kauli iliyomfanya Dk. Nagu kubainisha kwamba Mbilinyi alikuwa akizungumzia jambo ambalo hana uhakika nalo na kutaka aamriwe kuthibitisha.
Mwenyekiti Mabumba alikubaliana na hoja ya Dk. Nagu na alimtaka Mbilinyi kuthibitisha au kufuta kauli yake, Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu akaingilia kati akawasha kinasa sauti, lakini Mabumba alimwamuru akae chini, akakaa.
Kwa kweli sina lengo la kurudia yale yaliyotokea bungeni lakini ukweli ni kwamba tafrani ile ilihusisha wabunge wengi wa CCM na Chadema wakiwemo pia akina Stella Manyanya, John Mnyika na Mwigulu Nchemba. Hofu yangu ni namna wabunge wetu wanavyopotoka na kushindwa kujadili hoja kwa kutumia nguvu ya hoja jambo ambalo ni hatari.
Leo natoa ushauri kwa wabunge kuwa makini zaidi katika mijadala yao na kutambua kwamba , Bunge si uwanja wa malumbano ya kuendekeza siasa za vyama au itikadi zao, bali pamoja na mambo mengine ni jukwaa la kupokea, kuchambua kwa kina na kuyapatia ufumbuzi mambo mbalimbali yanayowahusu wananchi, yakiwemo yale yaliyogubikwa na utata.
Yapo mambo mengi ambayo hayajatafutiwa ufumbuzi na bunge kama vile sakata la David Jairo, fedha za EPA, matatizo ya madaktari, fedha za malimbikizo za walimu, wajiulize kwa nini kuna malimbizo ya fedha na kila mwaka wanaidhinisha fungu lao kwenye bajeti ya wizara ya elimu?
Niwashauri wabunge na viongozi wa Bunge kuwa chombo hiki adhimu, kisitekwe na hisia za vyama kwani tunavyoona sisi tulio nje ya bunge ni kwamba migawanyiko ya kiitikadi ipo wazi na vijembe hutawala wakati wa kujadili hoja au masuala nyeti ndani ya chombo hicho, kitu ambacho ni hatari na siyo haki kwa walipa kodi wanaotegemea matatizo yao yatafutiwe ufumbuzi.
Kitendo cha wabunge kulumbana hadi kufikia hatua ya kushindwa kuheshimu kanuni na taratibu za bunge, kinatia shaka na kuzua hofu kubwa kwa umma unaoamini kwamba wawakilishi wao hao ndiyo tiba ya matatizo yao. Hakika wanaoacha wajibu wao na kuanza malumbano yasiyo na tija kwa umma na kupoteza wakati kwa kupigana vijembe wajijue kuwa wanajitia aibu kwa jamii ya watu waliostarabika.
Wabunge nawashauri kuachana na ushabiki wa kisiasa kama ule wa mpira wa miguu ambapo huwa tunashuhudia timu moja inapofungwa, mashabiki wake huendelea kuamini kuwa timu yao ni bora kuliko wale waliowafunga na kwamba kulikuwa na njama za kufungwa kwao.
Bunge linatakiwa liwe sehemu ya kujadili hoja kwa misingi ya haki bila kutanguliza ushabiki wala kuzua malumbano yasiyo na tija kwa Watanzania na siyo sehemu ya kuonesha ujuzi wa kuzungumza, ni mahali pa kutoa hoja za msingi za kujenga nchi.
Wabunge wakumbuke kwamba, Watanzania wana imani na chombo hicho ndiyo maana wameridhia kodi zao zitumike, kwa manufaa ya maendeleo ya Taifa, hivyo ni dhambi kubwa kutumia muda wa walipa kodi kwa malumbano yasiyo na tija kwa Watanzania maana wakumbuke kuwa wapo ambao hawana vyama.
Ukweli ni kwamba suala la kutekwa na kuumizwa kwa Dk. Ulimboka sasa lipo mikononi mwa vyombo vya dola. Rais Jakaya Kikwete katika hotuba yake kwa taifa ya mwishoni mwezi uliopita, alilizungumzia kwa kina na kuwaahidi Watanzania kwamba ukweli utafahamika na kuviamuru vyombo husika, kuhakikisha vinafanya uchunguzi wa kina ili kuondoa utata uliopo.
Mimi naamini wabunge wanatambua kuwa wana jukumu kubwa kwa taifa na kamwe wanapokuwa kwenye mijadala yao, wasiongozwe na hisia wala jazba bali wawe na uhakika na yale wanayoyasema , kinyume na hapo chombo hiki kitapoteza imani kwa umma, kitu ambacho sitaki kitokee.
Jipu limepasuka, siwezi kuwa adui kwa kusema ukweli.