
WAZIRI
 Kivuli wa Fedha na Uchumi, Zitto Kabwe jana aliwasilisha bungeni bajeti
 mbadala ya Kambi ya Upinzani kwa mwaka wa fedha 2012/2013, huku 
akibainisha kasoro lukuki katika bajeti ya Serikali ilioyowasilishwa 
Alhamisi iliyopita.Bajeti ya Zitto ilitanguliwa na hotuba ya Msemaji 
Mkuu wa Kambi ya Upinzani kuhusu Ofisi ya Rais – Mipango, Christina 
Mughwai ambaye pia aliweka wazi kile alichokiita udhaifu wa Serikali 
katika kuitekeleza mipango yake ya kiuchumi, hali ambayo inasababisha 
umaskini kwa wananchi.
Hotuba
 zote mbili, ya Zitto na Lissu, zilisema licha ya Serikali kutangaza 
kwamba bajeti ya 2011/12 ilikuwa ya kupunguza makali ya maisha, hakukuwa
 na nafuu yoyote kwa wananchi kwani maisha yameendelea kupanda.
Pamoja
 na kupendekeza njia kadhaa za kupanua wigo wa mapato ya Serikali, 
wapinzani wametaka kufanywa kwa ukaguzi wa deni la taifa, ili kubaini 
chanzo cha Serikali kukopa na kuweka wazi jinsi fedha hizo zilivyotumika
 hadi kufikia Sh22 trilioni.
Zitto
 ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni katika hotuba yake 
alisema mapato ya Serikali yanaweza kuongezwa kwa Sh2.885 trilioni, 
hivyo kupunguza utegemezi wa mikopo ya kibiashara ambayo imekuwa 
ikiligharimu taifa kiasi kikubwa cha fedha.
Vyanzo
 vya kodi na kiasi cha fedha kwenye mabano alivyopendekeza ni 
marekebisho ya kodi za misitu ikiwamo mkaa (Sh130.8 bilioni), Kupunguza 
misamaha ya kodi, kuzuia ukwepaji kodi na udanganyifu wa biashara ya nje
 (Sh742.74 bilioni), Mauzo ya hisa za Serikali (Sh415.55 bilioni), 
Marekebisho ya kodi Sekta ya Madini na asilimia 25 ya Mauzo ya Madini 
Nje (Sh578.36 bilioni) na Marekebisho ya Kodi na Usimamizi bora wa 
Mapato Kampuni za Simu (Sh502.26 bilioni).
Mapendekezo
 mengine ni Marekebisho ya Kodi ya Tozo ya Kuendeleza Stadi (Sh243.52 
bilioni), mapato ya wanyamapori (Sh61.64 bilioni), kuondoa msamaha wa 
ushuru wa mafuta kwa kampuni za madini (Sh44.9 bilioni), Usimamizi wa 
mapato ya utalii (Sh51.75 bilioni), Kuimarisha biashara Afrika Mashariki
 (Sh 114.15 bilioni).
Zitto
 alisema kama wapinzani wangekuwa madarakani wangekusanya kiasi cha Sh15
 bilioni sawa na ile ya Serikali, lakini tofauti ni hatua ya kutenga 
asilimia 35 ya mapato ya ndani kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya 
maendeleo na kupunguza utegemezi wa bajeti kutoka asilimia 42.37 za 
Serikali hadi asilimia 21.3.
Deni la Taifa
Kuhusu
 deni la Taifa, mbunge huyo wa Kigoma Kaskazini (Chadema), alisema 
Serikali haipaswi kuendelea kukopa, kwani taarifa rasmi za kibenki na 
ukaguzi wa hesabu zinaonyesha kwamba deni hilo linakua kwa kasi tofauti 
na maelezo ya Serikali kwamba linahimilika.
“Taarifa
 ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali inaonyesha kuwa Deni 
la Taifa linazidi kuongezeka kwa asilimia 38 kutoka Sh10.5 trilioni 
mwaka 2009/2010 hadi Sh14.4 trilioni 2010/2011. Kwa mujibu wa Waziri wa 
Fedha, Deni la Taifa limefikia Sh20.3 trilioni mpaka ilipofika mwezi 
Machi mwaka 2012,”alisema Zitto na kuongeza:
“Ukisoma
 taarifa ya Mwezi wa Mei 2012 ya Benki Kuu ya Tanzania, Deni la Taifa 
sasa limefikia Sh22 trillion. Suala hapa sio ustahmilivu wa Deni kama 
inavyodai Serikali, bali ni kwamba tunakopa kufanyia nini?”
Alisema
 hesabu za bajeti ya Serikali ya 2012/13 inayopendekezwa zinaonyesha 
kwamba Serikali bado ina mpango wa kukopa kwa ajili ya kugharamia 
matumizi ya kawaida ambayo hayazalishi wala kutozwa kodi.
“Hatutaki
 mikopo kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya posho, kusafiri, magari n.k.
 Tuchukue mikopo kuwekeza kwenye miradi itakayokuza uchumi na kuzalisha 
kodi zaidi,” alisema.
Kuhusu
 mfumuko wa bei, Zitto alikosoa hatua zinazopendekezwa na Serikali 
kukabiliana nao, kwamba ni zile zilizoshindwa katika mwaka wa fedha 
unaoishia Juni 30, mwaka huu. kutoka Mwananchi. www.mwananchi.com
 
