Friday, July 27, 2012

SHARO MILIONEA ADAIWA KUTAPELI


Hussein Mkiety ‘Sharo Milionea’.
Na Erick Evarist
MWANAMUZIKI ambaye pia ni mchekeshaji Bongo, Hussein Mkiety ‘Sharo Milionea’ juzikati ameshutumiwa kutapeli mkwanja wa shoo.
Chanzo chetu cha kuaminika kimedai kuwa, Sharo Milionea hivi karibuni alikubaliana na promota aitwaye Christopher Nicolous kwenda kupiga shoo tatu katika Wilaya ya Ifakara mkoani Morogoro ambapo alipokea ‘advance’ ya shilingi laki 6 kati ya laki 9 aliyotakiwa kulipwa.
Ikadaiwa kuwa, ilipofika siku ya shoo, msanii huyo alikataa kuingia mzigoni baada ya kubaini kuwa anakotakiwa kwenda kupiga shoo ni mbali kutoka Ifakara mjini.
“Jamaa walimpa laki sita, tayari na matangazo kibao walishalipia lakini alipofika na kuambiwa ajiandae kwa shoo, akachomoa kufanya shoo tatu kwa madai kwamba aongezewe mkwanja,” alisema mtoa habari huyo.
Ijumaa lilimtafuta Sharo Milionea kuzungumzia ishu hiyo na alipopatikana alisema: “Jamaa walinilazimisha kwenda mbali zaidi tofauti na makubaliano mi’ nikakataa, nikawarudishia mkwanja wao wa advance, wanasema nimewatapeli kwa kuwa niligoma kuwarudishia fedha za matangazo walizotaka nilipe.”